Friday, July 26, 2013

Wazee waliopigana vita kuu wailalamikia serikali



Wazee waliopigana Vita Kuu ya Pili ya Dunia wameilalamikia Serikali wakisema haionyeshi kuwajali licha ya kutoa mchango mkubwa kwa taifa.
Wakizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Mashujaa ambayo kimkoa yaliadhimishwa katika Viwanja wa Naliendele na kuhudhuriwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia, wazee hao walidai kwamba Serikali imekuwa ikipokea misaada kwa ajili yao lakini imekuwa haiwafikii.
Mmoja wa wazee hao, Vicent Mshamu (91), alisema Serikali haiwasaidii kitu chochote licha ya wahisani kutoa fedha za kuwasaidia kutokana na mchango walioutoa kwa taifa.
“Kuna fungu linatolewa na wahisani kwa ajili ya kutusadia lakini cha ajabu fungu hilo halitufikii sisi walengwa na hatujui jinsi gani fungu hilo la fedha linavyotumika ukizingatia kwa sasa hatuna nguvu wala mshahara. Ombi letu kwa Serikali ni kwamba iangalie namna ya kutusaidia na kutuenzi watu tulioshiriki katika vita,” alisema Mzee Mshamu.
Mshereheshaji wa maadhimisho hayo, Luteni Bariki Julius Mwakivega alisema Tanzania ilishiriki kikamilifu katika harakati za ukombozi wa Msumbiji kuanzia mwaka 1970.
Alisema kuwa Jeshi hilo lilishiriki katika operesheni mbili, Tegema iliyofanyika katika Jimbo la Tetegaza na Manica na operesheni Safisha katika Jimbo la Zambezia.
Alisema wapiganaji 101 walioshiriki katika harakati za ukombozi wa Msumbiji walipoteza maisha na kuzikwa nchini humo kabla ya mwaka 2004. Serikali ya Tanzania na ile ya Msumbiji ziliamua kurejesha miili ya mashujaa hao katika ardhi ya nchi yao na kuzikwa katika eneo la jeshi la Naliendele.
 Source : mwananchi

0 comments:

Post a Comment